Kuzama kwa boti ambamo wahamiaji
wapatao 400 wanahofiwa kufa wiki hii katika pwani ya Libya kulitokana na
furaha ya kushangilia kwa kuona meli ya uokoaji.
Watu
walionusurika katika ajali hiyo wamewaambia maafisa kwamba boti ilizama
wakati wahamiaji wengi walipohamia upande mmoja wa boti walipoona meli
ya uokoaji ikiwakaribia.Kuzama kwa boti hiyo Jumatatu ni miongoni mwa jali mbaya kuliko zote kutokea katika bahari ya Mediterani.
Mashirika ya misaada yamesema jitihada za kuokoa maisha ya watu hazitoshelezi kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu wanaotaka kuvuka kwenda Ulaya.
Watu wapatao 10,000 wameokolewa katika siku za hivi karibuni, na boti zaidi zinaelekea katika pwani ya Italia.
Walinzi wa pwani ya Italia waliwaokoa watu wapatao 140 kutoka katika boti iliyozama Jumatatu. Watu walionusurika wanasema zaidi ya watu 500 walikuwa katika boti hiyo wakati inazama.
Msemaji wa shirika la kimataifa la wahamiaji, Joel Millman, menukuliwa na shirika la habari la Uingereza, Reuters akisema theluthi moja ya watu hao ni wanawake na watoto.
Zaidi ya watu 500 wamekufa wakijaribu kuvuka bahari ya Mediterani tangu kuanza kwa mwaka huu, ikiwa ni mara 30 zaidi ya vifo vilivyotokea mwaka jana katika kipindi kama hicho.
Kama idadi ya watu waliokufa kutokana na ajali ya hivi karibuni itathibitika, idadi ya vifo kwa mwaka huu itaongezeka kufikia watu 900.
No comments:
Post a Comment